ads

adds

SVEN NA MATOLA WATOA MAAGIZO MAKALI BAADA YA USHINDI


Licha ya kuwapongeza kwa kucheza vizuri katika ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Mwadui FC kocha mkuu, Sven Vandenbroeck amewataka wachezaji wake waendelee kujituma katika mechi zinazofuata ili watangaze ubingwa mapema. Ujumbe huo unatokana na ratiba yetu ilivyo kwakua mwanzoni mwa mwezi ujao tutakuwa na mchezo mgumu wa robo fainali ya michuano ya FA dhidi ya Azam FC ambapo Sven anataka mpaka muda huo tuwe tumetawazwa mabingwa. Kocha Sven amesema amefurahi kuona wachezaji wake wakishika mafunzo ya kubadili mfumo wa uchezaji kwa haraka ndani ya siku tatu na kuutumia vema uliopelekea kupatikana kwa ushindi huu mnono. "Ujumbe wangu kwa wachezaji ni kuwataka kuendelea kujituma, kujitoa kwa ajili ya timu ili tutangaze ubingwa mapema. Tutakuwa na ratiba ngumu kuanzia mwanzoni mwa mwezi ujao," amesema kocha Sven. Kwa upande wake kocha msaidizi, Suleiman Matola amewapongeza wachezaji kwa kucheza vizuri huku akiwataka wafanye hivyo katika mechi zijazo dhidi ya Tanzania Prisons na Mbeya City. "Nichukue nafasi kuwapongeza wachezaji kwa kucheza vizuri na kufanikiwa kupata ushindi mnono, kikubwa nawataka wasibwete twende Mbeya tukafanye kama tulichofanya kwa Mwadui," amesema Matola.

Post a Comment

0 Comments