NONDO NJIA NYEUPE KUTUA SIMBA


Uongozi wa Coastal Union umesema kuwa wapo tayari kumuuza beki wao chipukizi Bakari Nondo ambaye pia ni nahodha wa kikosi hicho chenye maskani yake Tanga kwa Simba iwapo watafikia makubaliano.

Nondo amekuwa moto msimu huu ndani ya Coastal Union jambo ambalo limewafanya mabosi wa Simba kuiwinda saini yake ili avae jezi yenye rangi nyekundu. 

Mjumbe wa Kamati ya Usajili ya Coastal Union, Ahmad Aulora amesema kuwa hawana tatizo iwapo Simba itawafuata ili kumalizana nao kuhusu beki wao huyo.

"Bado ni mchezaji wa Coastal Union lakini haina maana kwamba tutaweza kumzuia kuondoka ndani ya timu yetu kwani kazi ya mchezaji ni kucheza mpira.

"Iwapo watakuja mezani tukazungumza basi itakuwa ni ruksa kwake kucheza ndani ya timu ambayo inamtaka hata ikiwa ni Simba haina tatizo," amesema.

Kwenye safu za ulinzi ambazo zimeruhusu mabao machache Coastal Union ni namba mbili ambapo imefungwa mabao 19 huku ya kwanza kufungwa mabao machache ni Simba imefungwa mabao 15.

Post a Comment

0 Comments