HUYU HAPA NDIYE MBADALA SAHIHI WA TSHISHIMBI


Kumekuwa na mjadala mkali miongoni mwa wadau wa klabu ya Yanga wengi wakionekana kutofurahishwa na kitendo cha nahodha wao Papy Tshishimbi 'kusuasua' kusaini mkataba mpya

Hivi karibuni Afisa Habari wa Yanga Hassan Bumbuli alidokeza kuwa Tshishimbi alipewa ofa nono hivyo wanaamini atasaini mkataba huo hasa ikizingatiwa kocha Luc Eymael amependekeza Mcongoman huyo abaki

Lakini hata ikitokea Tshishimbi akaondoka Yanga, mabingwa hao wa kihistoria sidhani kama watatetereka

Miongoni mwa wachezaji wanaohusishwa kuchukua nafasi yake ni kiungo mkabaji wa Mtibwa Sugar Abdulkarim Humud

Kama Yanga itafanikiwa kumpata mwamba huyu, basi Wanayanga watamsahau Tshishimbi haraka sana Iko hivi, kwa mfumo ambao kocha Luc Eymael anatumia sasa, majukumu ya Tshishimbi yako zaidi kwenye kuilinda safu ya ulinzi, na wakati mwingine kuanzisha mashambulizi

Ukiangalia kwenye mchezo dhidi ya Simba ambao Yanga ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0, Eymael alibadili mfumo wake kutokana na aina ya wachezaji aliokuwa nao na hii inatoa taswira ya mwelekeo wa Yanga jinsi itakavyokuwa ikicheza

Ukiangalia katika mechi ile aliyen'gara zaidi kwenye safu ya kiungo ni Feisal Salum 'Fei Toto'. Fundi huyu wa mpira kutoka visiwani Zanzibar pengine ndiye aliyepata alama nyingi zaidi miongoni mwa viungo wote wa Yanga na Simba waliiocheza siku ile

Fei Toto alikuwa hatari kwelikweli, ndio maana kuna wakati Clatous Chama alimfanyia madhambi ya makusudi kabisa, tukio ambao pengine lingeweza kumaliza maisha yake ya kusakata kabumbu

Huyu Fei Toto kwa sasa mfukoni mwake ndio anatembea na ramani yote ya mchezo wote wa Yanga

Baada ya Eymael kubaini ni mchezaji fundi kwelikweli, mwenye uwezo mkubwa wa kupiga pasi makini tena hata akiwa umbali mrefu, amempa jukumu hilo zito

Eymael anamtumia Fei Toto kama kiungo mkabaji 'fake' lakini kazi yake kubwa ni kuchezesha timu kutokea nyuma akishirikiana vyema na Haruna Niyonzima anayecheza juu yake

Kwenye mchezo dhidi ya Simba alicheza chini pamoja na Tshishimbi lakini yeye jukumu lake kubwa lilikuwa kuanzisha mashambulizi pale wanapopora mpira.Kazi zote 'chafu' zilikuwa zikifanywa na Tshishimbi,  Toto yeye alitumika zaidi Yanga inapokuwa na mpira, uwezo wake wa kupiga 'pasi rura' ilikuwa silaha muhimu

Turudi kwa Humudi
Humud amekuwa na msimu bora sana klabu ya Mtibwa Sugar, haishangazi kuona kocha wa Stars Etienne Ndayiragije alimuita kwenye kikosi chake kuchukua nafasi ya Jonas Mkude pale 'alipozingua' kabla Corona haijapelekea michuano ya CHAN kusitishwa

Kwa aina ya mfumo ambao Yanga wanacheza sasa, Humud anaweza kufaa zaidi pengine kuliko Tshishimbi ambaye huwa ana kawaida ya kutotulia katika eneo lake
Humud hana vitu vingi sana na pengine ndio maana mashabiki wengine wanambeza, lakini ni mchezaji ambaye akipewa kazi anaifanya ipasavyo

Nakumbuka Yanga ilipocheza na Mtibwa Sugar, Humud alijitahidi kwa kiasi kikubwa kuweza kumdhibiti Morrison, pengine ndio mchezaji ambaye Morrison anaweza kumtaja kuwa alimsumbua

Huyu ni mchezaji sahihi kusimama na Fei Toto, kwani uwepo wake utampa Fei Toto Uhuru wa kuichezesha timu

Ndio, Humud ana uwezo mkubwa zaidi linapokuja suala la kukaba, hapa anaweza hata kumzidi Tshishimbi

Ni mchezaji ambaye hana papara, sio muoga na ana uzoefu wa mikikimikiki ya mechi kubwa

Tanzania imejaliwa kuwa na wachezaji wengi sana wenye vipaji, bahati mbaya huwa hawaaminiwa lakini unakuta kazi wanayofanya wakati mwingine ni zaidi ya hata wachezaji wa kigeni wanaokuja kulipwa Mamilioni

Hii ni changamoto hata kwa Yanga, pengine kuna ulazima wa kurudisha kitengo cha 'scouting' ya wachezaji ambacho kinaweza kusimamiwa na wachezaji wa zamani

Post a Comment

0 Comments