SIMBA WAENDELEA KUMBANIA KOCHA WAO PATRICK AUSSEMS

 Mtendaji mkuu wa Simba Senzo Mazingisa amemkazia kocha mkuu wa timu hiyo, Mbelgiji, Patrick Aussems kwa kumsimamisha kazi hadi watakapomjadili huku kocha msaidizi.


Aussems amesimamishwa kuisimamia timu hiyo aliyoipa mafanikio msimu uliopita baada ya kuifikisha robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika kufuatia kuondoka nchini kimya kimya bila ya kutoa taarifa kwa waajiri wake kwa muda wa siku tatu hali iliyopelekea kukumbana na panga hilo.

Katika mazoezi yaliyofanyika juzi Jumanne kwenye Uwanja wa Gymkhana, Simba ilikuwa chini ya kocha msaidizi, Denis Kitambi mwenye leseni B ya Shirikisho la Soka Ulaya (UEFA) akisimamia mazoezi hayo kwa muda wa saa tatu kutoka saa tatu asubuhi hadi saa tano na dakika 30. Kitambi ni miongoni mwa makocha wachache wazawa wenye sifa za kimataifa.


amospoti.com ilikuwepo uwanjani hapo ilimshuhudia Kitambi, akisaidiwa na kocha wa viungo, Adel Zrane na kocha wa makipa Mohammed Mwarami ambapo alianza kwa kuwakimbiza wachezaji kwelikweli.

Kitambi aliwagawa wachezaji kwa makundi matatu ambao walikimbia katikati ya uwanja kwa spidi kubwa na ndogo kwa muda wa dakika 30 kabla ya kuwabadilishia mazoezi mengine ambayo yalitumia muda mwingi umilikiji wa mpira.

Lakini Kitambi ambaye alikuwa akisaidiwa na wasaidizi wake alitumia muda mwingi katika zoezi la kufunga mabao kwa kuwatumia, Meddie Kagere na Miraj Athuman ‘Sheva’ ambao walikuwa wakifunga kwa mpira ya krosi iliyokuwa ikipigwa na mawinga wa pembeni huku katika zoezi hilo kiungo Clatous Chama akifunga mabao matano wakati Kagere na Sheva wakifunga mabao mawili kila mmoja.

Kitambi alisema kuwa kwa sasa amekabidhiwa majukumu ya kuifundisha timu hiyo na mtendaji mkuu kwa muda wa wiki moja wakati wakisubiria mustakabali wa kocha mkuu Patrick Aussems aliyesimamishwa.

Kitambi alinukuliwa akisema “Nimekabidhiwa kusimamia majukumu na programu zote za timu na mtendaji mkuu kwa sababu mwalimu yeye amesimamishwa hadi pale watakapokaa chini na uongozi kumjadili.

“Hili ni jukumu la wiki moja kwa maelezo niliyopewa kwa kuwa mwalimu anakutana na uongozi kesho (leo) ili kujua kama ataendelea kuwepo au nini kitatokea, kikubwa mashabiki wawe watulivu wakati uongozi unajaribu kuweka mambo sawa,

Kitambi aliongeza kuwa: “Lakini kwa upande wa wachezaji hawapo sawa kisaikolojia kutokana na hali inayoendelea sasa ingawa naamini ni kitu cha kawaida na watakaa sawa.”

Post a Comment

0 Comments