advertise with us

ADVERTISE HERE

HATIMAYE JIBU LIMEPATIKANA KUHUSU MKAPA KUWA SHABIKI WA SIMBA AU YANGA

Niliwahi kuliona andiko kwa mchambuzi na mwandishi nguli wa magazeti Bw.Maggid Mjengwa akiuliza je Mkapa ni shabiki wa timu gani kati ya Simba na Yanga ?

Hatimaye mchambuzi huyo amepata jibu la swali lake na ameliandika kama ifuatavyo. Maggid Mjengwa anaanza kwa kuweka picha ya kitabu cha mkapa cha "My life ,My Purpose" na  anasema :

Kitabu kinatoa jibu kuwa Ben Mkapa hakuwahi kupenda kushiriki michezo.
Kwa ukaribu kwenye mpira aliwahi kuwa kiongozi wa ushangiliaji/ Uhamasishaji nje ya uwanja akiwa Pugu Sekondari ( St Francis).
Ndugu zangu,
Kwa kukisoma kitabu cha Mkapa ‘ My Life, My Purpose’, naweza kusema hapa, kuwa Ben Mkapa anabainisha kuwa hakuwahi kupenda kushiriki michezo na wala si mpenzi wa mchezo wa mpira wa miguu.
Anakiri, kuwa umbile lake dogo akiwa Sekondari Ndanda, lilimfanya asifikiriwe na wenzake kuingizwa uwanjani. Kila darasa Mkapa ndiye aliyekuwa mdogo kuliko wenzake. Alikuwa mwembamba pia.
Anakumbuka tu akiwa Pugu Sekondari, kuwa alikuwa ‘ Cheering leader’ kiongozi wa ushangiliaji/ uhamasishaji nje ya uwanja timu yao ilipocheza mechi. Na alikuwa na maneno sana nje ya uwanja mpaka hutokea mwalimu wao akamwambia; “ We Ben, funga mdomo wako!”
Kwa maneno mengine, enzi zake pale Pugu Sekondari Ben Mkapa alikuwa ni kama tu Haji Manara wa Simba!
Naam, kwenye utawala wake, Benjamin Mkapa hakupata kuonekana kwenye viwanja vya soka.
Ajabu ya Mkapa, wakati wananchi wake wakitafakari juu watafanyaje na uwanja wao wa taifa uliochakaa, ni Benjamin Mkapa aliyeahidi kuwajengea uwanja wa kisasa kabla hajamaliza muda wake, na akatimiza ahadi yake hiyo.
Nchi yetu kwenye kandanda kimsingi imegawanyika kati ya Simba na Yanga. Na viongozi wetu pia. Kama tulivyokuwa hatujui kama Nyerere alikuwa Simba au Yanga ndivyo ilivyokuwa kwa Mkapa.
Akiwa Rais Mstaafu, mwaka 2008 Benjamin Mkapa aliongea kwenye Ubalozi wa Finland. Ikaandikwa, " Mkapa atoa neno!" Ni kwenye moja ya magazeti yetu. Hilo " neno alilotoa" mara ya mwisho kuhusu kandanda ni wakati alipowaaga pale Ubalozi wa Finland, watoto wa kutoka kwao Mtwara waliokuwa safarini kwenda Finland kucheza soka.
Kuongea kule kwa Mkapa kulikuwa na tofauti kubwa. Ikaripotiwa, kuwa Mkapa kaongea kuhusu michezo. Habari ikawa kubwa na maswali mitaani yakaendelea kuulizwa, na swali kuu lilikuwa;
" Jamani hivi Mkapa Simba au Yanga?
Waliokuwepo pale Ubalozini kuna waliomsikia Mkapa akitamka kupenda alama ya Simba katika michezo. Kuna mwandishi mwingine aliyeandika kuwa ni kweli Mkapa aliulizwa swali na mmoja wa watoto hao kuwa anapenda timu gani.
Mwandishi huyo akaandika, kuwa Mkapa alimjibu mtoto huyo
" Wee, acha utundu!"
Swali likabaki, Mkapa Yanga au Simba?
Na kitabu chake kimekuja na jibu.Kuwa Mkapa si Yanga wala Simba. Na yawezekana Mkapa hajui hata kama kuna timu inaitwa Namungo FC kule Ruangwa jirani na shule yake ya zamani ya Ndanda!
Maggid Mjengwa.

Post a Comment

0 Comments